Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Bungu, Dismas Kimweli.
  Baadhi ya wanafunzi wa shule ya sekondari Bungu wakiwa katika ofisi za 
walimu kuzungumzia mafanikio na changamoto mbalimbali  kitaaluma katika 
shule hiyo.
Baadhi ya wanafunzi wa shule ya sekondari Bungu wakiwa katika ofisi za 
walimu kuzungumzia mafanikio na changamoto mbalimbali  kitaaluma katika 
shule hiyo.
 
Kibao cha Shule ya Sekondari ya Bungu.
Na Mwandishi wa Thehabari.com, Korogwe
SUALA la kuwepo na utata kwa baadhi ya 
wanafunzi kukwamishwa na fomu namba 9 ya Takwimu za Shule za Msingi kwa 
mwanafunzi (TSM9) kufanya mitihani yao katika shule anuai za sekondari 
limezua mvutano kati ya wazazi wa wanafunzi na walimu huku kila upande 
ukitupa lawama kwa mwenzake.
 
Baadhi ya wanafunzi na wazazi waliohojiwa wamedai uzembe upo kwa walimu 
ambao hutumia majina ya wanafunzi wengine kuingiza wanafunzi kinyemela, 
jambo ambalo huzua utata baadaye kwa mwanafunzi aliyeingia kwa njia hiyo
 anapokaribia kufanya mitihani yake.
 
Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa habari hizi wilayani Korogwe katika
 shule kadhaa za sekondari na msingi umebaini kuwa wapo wanafunzi ambao 
wamezuiwa kufanya mtihani wa mwisho wa kidato cha nne na ule wa kidato 
cha pili wa mchujo kutokana na hali kama hiyo ya utata katika suala hilo
 la TSM9.
 
Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Bungu, Dismas Kimweli ambaye shule yake 
ilikuwa miongoni mwa shule zilizolalamikiwa, akizungumza na mwandishi wa
 habari hizi alipinga kuwepo na wanafunzi waliozuiliwa kufanya mitihani 
yao kutokana na utata wa fomu namba 9.
 
Mwalimu huyo alisema idadi kubwa la wanafunzi ambao hukumbwa na matatizo
 kama hayo ni wanafunzi ambao huingia shuleni kwa njia ya uhamisho huku 
wazazi wao wakiomba mwanafunzi aendelee kusoma wakati utaratibu wa 
kufuatilia uhamisho ukiendelea.
 
“Unakuta mzazi anamleta mtoto kujiunga na shule yako akitokea shule 
nyingine na anaomba aendelee kusoma wakati akiendelea kufuatilia 
uhamisho...lakini baadaye anakaa kimya sasa mtoto anakuwa anaendelea na 
shule bila kuwa na uhamisho ambao hujumuisha TSM9, ikifika kipindi cha 
mitihani hapo linakuwa tatizo na mzazi anajifanya kasahau,” alisema.
 
“Sasa kama mtu hajatimiza vitu kama hizi anarushaje lawama kwa walimu au
 shule...lakini ikifikia hatua hii wapo ambao huwaeleza nao kuelewa na 
wapo ambao huwa na mvutano kidogo,” aliongeza mwalimu huyo.
 
Akitoa ufafanuzi wa suala hilo, Kaimu Ofisa Elimu Sekondari Halmashauri 
ya Wilaya ya Korogwe, Shaban Shemzighwa alikiri kuwepo kwa malalamiko ya
 baadhi ya wanafunzi kutokuwa na TSM9 hasa wa kidato cha pili lakini 
alidai waliruhusiwa kufanya mitihani yao na wao kuwaagiza wakuu wa shule
 wanazotoka kuhakikisha wanawasilisha namba zao kwenye vituo 
inakosahishiwa mitihani.
 
“Taarifa za malalamiko zilitufikia na baadhi ya Shule za Sekondari 
ambazo wanafunzi walikuwa na matatizo hayo ni Bungu, Patema, Mfundia na 
nyinginezo, hapa nipo nje ya kituo cha kazi hivyo ni vigumu kutaja idadi
 na shule zote,” alisema Shemzighwa akizungumza na mwandishi wa habari 
hizi kwa njia ya simu.
 
Aidha akifafanua zaidi alisema wanafunzi wengi waliokuwa na matatizo 
kama hayo wa kidato cha pili ni wale waliohama kutoka shule moja kwenda 
nyingine, ambao hawakuja na TSM9 zao. “…Hata hivyo waliruhusiwa kufanya 
mitihani na maelekezo tuliwapa wakuu wa shule kuhakikisha wanapeleka 
namba za wanafunzi hao katika kituo cha kusaishia mitihani ili waweze 
kutambuliwa kihalali vinginevyo hawawezi kutambulika,” alisema ofisa 
huyo.
 
Alisema inaonekana kuna baadhi ya walimu wakuu walipokea wanafunzi bila 
TSM9, hata hivyo haikujulikana kama ni kwa njia ya kinyemela au matatizo
 ya uhamisho kwa wanafunzi hao kutoka shule moja hadi nyingine. Hata 
hivyo licha ya kiongozi huyu kuitaja Bungu kuwa miongoni mwa shule 
zilizotolewa tarifa kuwa na tatizo la fomu namba 9, mkuu wa shule hiyo 
alipinga shule yake kuwemo.
*Imeandaliwa na Thehabari.com kwa ushirikiano na HakiElimu
 
 
No comments:
Post a Comment