Zitto Kabwe
Maandamano
 ya amani yaliyofanyika mjini Mtwara siku ya alhamis wiki hii yameibua 
hoja mbali mbali kutoka kwa viongozi, wananchi, vyombo vya habari na 
mjadala wa siku nzima kwenye mitandao ya kijamii hasa facebook, twitter 
na JamiiForums. Mkuu wa Mkoa wa Mtwara ameita waandamanaji wapuuzi na 
Waziri wa Nishati na Madini amewaita watu hatari na wahaini. CHADEMA 
tumetoa kauli kupitia kwa Waziri Kivuli wa Nishati na Madini kwamba 
udhaifu wa utendaji serikalini ndio chanzo cha maandamano haya.
Lakini 
kuna tatizo kubwa zaidi ambalo linaonekana siyo katika sekta hii tu bali
 pia katika sekta nyingine ambapo tunaona matokeo yake katika maisha ya 
watu wetu na naweza kusema ni dalili za kushindikana kwa sera za CCM. 
Sera hizi ndizo ambazo zimelifikisha taifa hili hadi hapa. Kama hadi 
wananchi wa Mtwara ambako kwa muda mrefu imekuwa ni ngombe ya CCM 
wanaanza kuhoji matokeo ya sera za chama tawala basi ni dalili kuwa 
Watanzania wamefungua macho yao na wanaona.
Wanaona 
katika nishati, wanaona katika utawala bora, wanaona katia elimu 
(kuanzia ya msingi hadi ya juu kabisa!), wanaona katika afya, wanaona 
katika utendaji wa jeshi la polisi wanaona katika madini. Sera za CCM 
zimeshindwa. Zimeshindwa kuinua maisha yao na zinaonekana kuendelea 
kushindwa.
Mtwara na Lindi wanataka nini?.
Watu wa 
Mtwara wanataka gesi isiondoke Mtwara na badala yake viwanda na mitambo 
ijengwe Mtwara kisha kama ni umeme au mbolea isafirishwe kupelekwa 
sehemu nyingine ya nchi. Watu wa Mtwara hawasemi kwamba Gesi yote na 
mazao yake vibaki Mtwara na Lindi. Wanasema umeme uzalishwe Mtwara 
usambazwe nchi nzima. Mbolea izalishwe Mtwara na kusambazwa nchi nzima. 
Wanataka Bandari ya Mtwara iboreshwe na kuhudumia mikoa ya Kusini. Watu 
wa Mtwara hawasemi kwamba mapato yote ya Gesi yatumike Mtwara tu la 
hasha.
Sio 
dhambi hata kidogo kwa watu wa Mtwara kudai masuala haya. Watu wa Mtwara
 wamefanya maandamano kwa amani kabisa bila kuharibu mali na kutoa maoni
 yao. Kwanini tuwasute na kuwasusubika kwa madai yao haya? Kwa nini 
tusiwasikilize? Kosa lao nini kudai viwanda ili wapate ajira? Tumesahau 
kuwa mikoa ya Lindi na Mtwara ni mikoa masikini kabisa nchini? 
Tumesahau
 kuwa mikoa ya Lindi na Mtwara ilitumika kwa ukombozi wa kusini mwa 
Afrika kiasi cha kuwa katika hatari kabisa? Tumesahau ‘sacrifice’ ya 
watu wa Mtwara na Lindi dhidi ya usalama wa nchi yetu? Tumesahau kuwa 
Korosho imekuwa zao kubwa la biashara na linaloingiza mapato mengi sana 
ya Fedha za kigeni? Waziri Muhongo anasema Mtwara warudishe Fedha za 
Mkonge na Kahawa. Mbona hataji fedha za Korosho? Mwaka 2011 Korosho 
ilikuwa zao la pili kwa kuingiza fedha nyingi za kigeni baada ya 
Tumbaku.
Lakini 
tujiulize, watu wa Mtwara na Lindi walifadi fedha za Mkonge? Walifaidi 
fedha za Kahawa? Wamefaidi fedha zao za Korosho? Tumesahau hata Reli 
iliyoachwa na Mkoloni ya Nachingwea – Mtwara iling’olewa na Serikali 
huru ya Tanzania?
Tujiulize
 zaidi, hivi watu wa Nzega wamefaidika vipi na Mgodi wa Resolute pale 
Lusu? Mgodi umefungwa ukiwa umezalisha na kuuaza dhahabu ya thamani ya 
dola za marekani 3.3 bilioni. Hivi katika uhai wa mgodi huu Serikali Kuu
 imekusanya kodi kiasi gani? Halmashauri ya Wilaya ya Nzega imepata 
ushuru kiasi gani? Watu wa Mtwara wanayaona haya yaliyotokea Nzega na 
yanayotokea Tarime, Biharamulo, Kahama na Geita. Watu wa Mtwara wana 
Haki kuandamana kuzuia haya yaliyotokea wenzao yasiwatokee wao kwenye 
Gesi asilia.
 
 
No comments:
Post a Comment