Sunday, December 30, 2012

MKUU wa Wilaya ya Handeni mkoani Tanga, Muhingo Rweyemamu, ametangaza kufunga ofisi yake kuanzia Januari 3, mwakani hadi Februari 3, atangaza kuhamia kwa wananchi mwezi mzima

 
Amesema lengo la hatua ni kusimamia kwa vitendo miradi inayohusu kilimo, elimu na ardhi, lengo ikiwa ni kuwaletea wananchi maendeleo.Muhingo katika mahojiano na simu na gazeti hili jana, alisema atatumia muda huo wa mwezi mmoja kusimamia kazi za maendeleo akianza na suala la kuhakikisha vyumba vya madarasa vinapatikana kwa ajili ya kuchukua wanafunzi wanaoanza darasa la kwanza na wanaojiunga na kidato cha kwanza. “Nitatembea katika tarafa zote saba za wilaya yetu.Nimemuagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya anipatie kila idara zinazohusika ofisa wa kuwa naye katika kazi hii. Kwa hiyo, nitakuwa na watu wa elimu, ardhi, kilimo, ufugaji wa nyuki na masuala ya wafugaji na wakulima.“Tunaanza na hili la madarasa kwa sababu sitaki mwanafunzi hata mmoja abaki nyumbani kwa kukosa madarasa ya darasa la kwanza na wale waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza,” alisema Muhingo ambaye kitaaluma ni mwalimu na mwandishi wa habari. Alisema katika kilimo, pia wataanza na shule 10 zilizoteuliwa kwa ajili ya kuendesha kilimo cha kisasa na hapo watatumia vocha 300 walizopewa na Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika na kila shule itakuwa na ekari 10, hivyo kufanya ekari 100. Alisema vocha hizo ni za mbegu, mbolea ya kupandia na kukuzia.Alisema mbali ya kupanda mahindi, pia shule hizo zitapanda mazao ya jamii ya mikunde na nia itakuwa ni kuhakikisha shule zinajitosheleza kwa chakula kwa ajili ya wanafunzi wake. “Namshukuru Waziri Mkuu na Wizara ya Kilimo kwa kutuletea vocha 300. Zitatusaidia sana. Ninataka Handeni inakuwa mfano katika mapinduzi ya kilimo, tukiamua tunaweza,” alisema Muhingo na kubainisha kuwa katika suala la kilimo, baadaye atakuwa na ziara wilayani Bagamoyo mkoani Pwani kujifunza kilimo cha mananasi.

No comments:

Post a Comment