Friday, December 28, 2012

Wanataaluma Wa Kiislamu Nchini (Tampro) Kusaidia Wanafunzi Sekondari Za Kata

Tampro ni Jumuiya isiyo ya kiserikali iliyoanzishwa mwaka 1994 na kusajiliwa rasmi serikalini Agost 22, 1997 ikiwa na malengo  mengi na mojawapo ni kufanya tafiti, kutoa mafunzo na ushauri wa kitaalam katika maeneo mbalimbali  ya maendeleo ya jamii.

JUMUIYA ya wanataaluma wa Kiislamu nchini (Tampro), imesema kwa kushirikiana na taasisi nyingine, inaandaa mpango mkakati wa kuhakikisha inawasaidia vijana wanaosoma katika shule za sekondari za Kata ili waweze kufanya vizuri katika mitihani yao ya mwisho kama sehemu ya jitihada zao kwa jamii ya Watanzania.
Akizungumza kuhusu  maazimio ya mkutano mkuu wa jumuiya hiyo uliomalizika juzi katika hotel ya Lamada jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji Jumuiya hiyo Sadiki Gogo, alisema wamefikia uamuzi huo baada ya kuridhika na utafiti ilioufanya na kubaini kuna haja ya wao kama wanataaluma kutafuta njia ya kuwasaidia vijana hao kimasomo.
 
”Tampro kupitia kliniki yake ya Elimu, iliomba na kupata kibali Wizarani cha kufanya utafiti katika shule kadhaa za sekondari za kata hapa nchini na kugundua kuwa zina uwezo wa kufanya vizuri iwapo zitasaidiwa katika baadhi ya nyanja” alisema Gogo
Akifafanua baadhi ya nyanja hizo, Mkurugenzi  huyo, alisema  pamoja na kuwapa mafunzo maalum walimu wa shule hizo na baadae kupeleka walimu wa kujitolea katika baadhi ya shule zitakazoonekana zina upungufu mkubwa.
 
Sambamba na mkakati huo ambao amedai unalenga kuisaidia serikali, Gogo alisema Tampro kupitia mkutano huo imeazimia kuanzisha vituo vya Elimu maalum pamoja na huduma nyinginezo kwa watu wenye mahitaji maalum kama vile ya ulemavu.
 
Aidha Mkutano mkuu huo umeazimia kushirikiana na wadau wengine nchini kuwekeza katika sekta ya Afya kwa madai kuwa bila ya kuwa na watu wenye afya zilizoimarika ,ni ngumu Taifa kufikia maendeleo ya kisiasa na kiuchumi.

Umoja Wa Makanisa Nchini Kuliombea Taifa Disemba 31 Uwanja Wa Taifa

NA : MWANDISHI WA FULLSHANGWE-DAR ES SALAAM

MUUNGANO wa Makanisa nchini unatarajia kufanya Mkesha wa kuliombea Taifa ili amani na utulivu uliopo uweze kudumu, ambao unatarajiwa kufanyika Desemba 31 mwaka huu kwenye viwanja vya Taifa jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na wandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo, Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi, Godfrey Malassy , alisema mkesha huo umekuwa ukifanyika kila Desemba 31 ya kila mwaka, kuukaribisha mwaka mpya.
 
Alisema lengo la mkesha huo ni kuliombea Taifa hilo mungu, ili aweze kuliponya na kulinusuru na majanga mbalimbali, na kudumisha amani miongoni mwa jamii yote nchini.
 
Malassy aliongeza kuwa Taifa kwa sasa linapita katika kipindi kigumu hususani kuanzia uelewa, uchumi, na katika masuala ya usalama wa raia wa ndani na nje ya nchi ambapo kuna baadhi ya watu wameanza kuichezea amani kwa kusababisha vurugu kwa kvisingizio vya dini.
 
Pia alisema kuwa Watanzania wanapaswa kudumisha amani na utulivu kwani hiyo ni tunu ambaayo wamepatiwa na mungu hivyo haipaswi kuchezewa na watu wachache wasio na nia njema.
 
“Mkesha wa dua hilo, utafanyika Desemba 31 mwaka huu kuanzia saa 2:00 usiku hadi asubuhi katika viwanja vya Taifa Dar es Salaam, na tunatarajia Rais Jakaya Kikwete atakuwa mmoja wa wageni wetu waalikwa” alisema Malassy.
 
Malassy alibainisha kuwa mkesha huo wa maombezi utashirikisha mikoa zaidi ya 16 ya Tanzania Bra na Visiwani, ambapo utakuwa na lengo la kuwaleta Watanzania kuliombea Taifa kwa ajili ya kudumisha amani, umoja na mshikamano visitetereke.

Maamuzi Ya Baraza La Madaktari Juu Ya Madaktari Waliogoma

Kutokana na mgomo wa madaktari uliotokea kati ya tarehe 23 na 29 mwezi
juni 2012.Wizara iliwasilisha malalamiko kwenye Baraza la madaktari
Tanganyika ili lifanye uchunguzi kuhusu madaktari hao .Idadi ya
madaktari wote waliogoma walikuwa 394, kati yao madaktari 376 walikuwa
ni madaktari walio katika mafunzo kwa vitendo (Interns) kutoka
hospitali za Muhimbili, K.C.M.C. Bugando, Mbeya Rufaa, St.Francis -
Ifakara, Dodoma, Temeke, Mwananyamala, Amana, Haydom na Sekou Toure.
Aidha, Madaktari waajiriwa(Registrar) 18 walishiriki katika mgomo huo
kutoka hospitali ya Rufaa ya Mbeya.


 Baraza lilipitia malalamiko yote na limetoa adhabu stahiki kwa kila
daktari aliyethibitishwa kushiriki katika mgomo huo.  Adhabu hizo
zilikuwa katika makundi yafuatayo; onyo, onyo kali na kusimamishwa
udaktari kwa muda wa kati ya mwezi mmoja na miezi sita.Vile vile kuna
Madaktari ambao hawakuwa na hatia ya kushiriki katika mgomo na hivyo
walifutiwa mashtaka.

MCHANGANUO WA ADHABU


•       Waliofutiwa mashitaka madaktari 49

•       Waliopewa onyo  madaktari 223
•       Waliopewa onyo kali madaktari 66
•       Kusimamishwa kwa muda madaktari 30
•       Mashitaka yaliyoahirishwa kutokana na wahusika kuhitaji ushauri wa
kisheria madaktari 4
•       Mashitaka yasiyosikilizwa kutokana na wahusika kutofika walipoitwa
na Baraza madaktari 22

Wizara inakamilisha taratibu za kinidhamu kwa mujibu wa Kanuni za

Utumishi wa Umma kwa Madaktari wote waajiriwa ambao walipatikana na
hatia mbele ya Baraza la Madaktari.   Wizara pia imeridhia kuwapa
Madaktari waliokuwa katika mafunzo kwa vitendo fursa nyingine ya
kuendelea na mafunzo hayo katika hospitali za Umma walizokuwepo kabla
ya kuondolewa.  Hata hivyo fursa hii haitawahusu Madaktari wote
waliopewa adhabu za kusimamishwa na Baraza la Madaktari, hadi hapo
watakapomaliza kutumikia adhabu zao.

HITIMISHO

Kwa taarifa hii madaktari wote waliofutiwa mashtaka na wale waliopewa
onyo na onyo kali wanatakiwa kuwasilisha kwa Katibu Mkuu Wizara ya
Afya na Ustawi wa Jamii barua kutoka kwa msajili wa Baraza la
Madaktari ikithibitisha kurejeshewa usajili  na kuruhusiwa kuendelea
na mafunzo kwa vitendo. Vile vile madaktari waajiriwa(Registrar)
wanatakiwa pia kuripoti kwa Katibu Mkuu Wizara ya Afya ili kupewa
barua zao kulingana na Adhabu walizopewa.  Barua hizi zitatolewa
kuanzia tarehe 2 Januari, 2013.Madaktari wote walio katika mafunzo kwa
vitendo wanatakiwa kuanza kazi katika vituo vyao vya awali  ifikapo
tarehe 14 Januari, 2013.Hakuna muda utakaoongezwa kwa kipindi
kilichobakia cha mafunzo kwa vitendo. Kwa wale wote waliopewa adhabu
wataanza kutumikia adhabu hizo kuanzia tarehe ya adhabu hiyo
ilivyotolewa.

Nsachris Mwamwaja

Msemaji
WIZARA YA AFYA NA USTAWI  WA JAMII
27/12/2012

Nguvu Ya Rangi Katika Biashara Zetu

Na: Albert Sanga, Iringa.
Leo nitawapitisha wajasiriamali katika somo muhimu kuhusu rangi. Je, unafahamu chimbuko la neno yeboyebo hapa nchini? Twende pamoja. Kampuni moja ya nchini Tanzania miaka michache iliyopita imewahi kutambulisha bidhaa zake za juisi zilizokuwa zikifahamika kama “Yebo” Juhudi kubwa iliwekwa katika matangazo kutoa taarifa kwa watumiaji kuhusu uwepo wa bidhaa hizo.

 Juisi ile ilikuwa ni ya rangi ya njano na katika matangazo ya kwenye televisheni walikuwa wakitumika watu waliokuwa wamevaa kandambili za plastiki zenye rangi ya njano. Kwa sababu kandambili hizo ndio kwanza zilikuwa zinaingia sokoni zikabatizwa jina la yebo yebo.

Haikuishia hapo, neno ‘yebo yebo’ likawa linapewa kwa kila kitu chochote kilichoonekana kutumia ama kuwa na rangi ya njano. Timu ya mpira ya Yanga ilikuwa mmoja wa waathirika wa hali hiyo kwani ilibatizwa jina la Yebo yebo! 

Yebo yebo likajipatia urasmi wa ‘kiaina’ kutumika kwa ajili ya kumaanisha kitu kinachopatikana kwa wingi, kisicho na thamani kubwa na kinachodharaulika. Sina uhakika kampuni husika ilichukua hatua gani baada ya hapo kujisalimisha na hatari ya bidhaa zao kuchukuliwa “poa” kutokana na matangazo waliyoyabuni.


Ukifuatilia maarifa katika sayansi ya biashara utabaini kuwa tatizo la kuzuka kwa neno ‘yebo yebo’ halikuwa katika kandambili za plastiki wala halikuwa katika ubora wa bidhaa (kwa maana ya juisi yenyewe ukitoa ufungashaji) bali tatizo lilianzia katika rangi ya njano. Rangi ya njano ilipelekea kuzaliwa kwa dhana ya uyebo yebo kutokana na namna inavyotafsiriwa katika ubongo wa mtu.

Unapoona bidhaa yeyote ikiwa imefungashiwa kwa rangi za aina Fulani basi ujue jambo hilo halifanyiki kwa bahati mbaya bali linabeba maana kwa mtumiaji hata kama mtumiaji hajijui kwa nini anatumia bidhaa za rangi fulani na asitumie za rangi nyingine. 

Ukiangalia soda ya Seven Up kutoka kampuni ya Pepsi pamoja na soda ya Sprite kutoka kampuni ya CocaCola utaona kuwa soda hizi zina rangi nyeupe lakini zinafungashwa katika chupa za kijani, kwa nini?

Katika nchi nyingi masikini ikiwemo Tanzania, makampuni na wajasiriamali wengi wamekuwa hawatilii mkazo suala la rangi katika biashara zao. Hii inajumuisha katika bidhaa, mazingira ya huduma pamoja na rangi zitumikazo katika majengo ya kufanyia hizo biashara. Kupuuza suala la umuhimu wa rangi katika biashara kumepelekea wafanyabiashara na makampuni mengi kushindwa kukubalika miongoni mwa watumiaji.

Si kila rangi inafaa kupakwa katika kuta za duka, si kila rangi inafaa kutumika katika kuandika maandishi kwenye vifungashio vya bidhaa. Umakini wa kuzingatia athari za rangi miongoni mwa watumiaji kunatajwa kuwa ni moja ya sababu zinazosababisha bidhaa kutoka nje ya Tanzania kupendwa ukilinganishwa na za hapa nyumbani.

Kimsingi rangi zimethibitishwa kuwa na uwezo wa kushawishi saikolojia pamoja na tabia za watu.  Mtaalamu mmoja wa saikolojia, Ward aliwahi kuulizwa njia za kuwezesha wafanyakazi kupunguza misongo wakiwa kazini.  Alijibu, “Haihitaji semina wala mafunzo, jambo la msingi ni kupaka rangi sahihi katika kuta za vyumba wanamofanyia kazi, ambayo itaweka hamasiko ama mfifio kwa mabadiliko yanayohitajika”

Kwa mujibu wa mtafiti mwingine wa mambo ya biashara katika masoko, Wexner, anabainisha kuwa rangi nyekundu kwa mfano inatajwa kuwa inaambatana na hisia za kuhamasika, machungwa inaambatana na kukatishwa tamaa na kudharauliwa.  Zambarau inaonesha hali ya kuthaminiwa, njano inawakilisha hali ya furaha, mzaha na kicheko na nyeusi inaonesha nguvu, umiliki na uimara.


Makampuni na biashara mbalimbali duniani kila siku zinakazana kutafuta njia za kuwezesha mwonekano na nguvu za nembo zao. Njia thabiti zinapovumbuliwa mikakati ya kimasoko huwekwa ambayo inahakikisha kuwa nembo hizo zinakuwa katika akili na fikra za wateja. 

Tofauti za kiutamaduni, kiuchumi, kijamii na nyinginezo zinaleta changamoto ya ugumu kwa biashara na makampuni kufahamu kwa usahihi aina moja tu ya nembo ambayo itawaridhisha na kuwapendezesha wateja wote. Hivyo biashara nyingi hasa za kimataifa zinajikuta kuwa zinalazimika kuwa na nembo moja katika muundo tofauti tofauti ili kufanikisha ufikaji wa bidhaa kama ilivyokusudiwa.


Mbinu mojawapo ya kimasoko inayotumika na waendeshaji wa masoko hasa kimataifa bila kujali eneo ama watu gani wanaoenda kutumia bidhaa hizo ni rangi. Rangi ni moja ya vifaa ambavyo mameneja masoko hutumia katika kutengeneza, kuimarisha na kurekebisha mwonekano wa nembo katika ufahamu wa mteja. Umuhimu wa rangi kuwasilisha maana Fulani kwa walengwa kunathibitishwa hata katika taratibu na sheria mbalimbali duniani.

Kwa mfano kule nchini Marekani kuna sheria inayofahamika kama Lanham Act ambayo inalinda rangi za bidhaa kama nembo halali za kibiashara . Rangi zinafahamika kuwa zinabeba chembechembe za kihisia na kisaikolojia. 

Maana mbalimbali zinazoambatana na rangi mbalimbali zinaumaana mkubwa sana kwa watu wanaohusika na masoko katika bidhaa ama huduma za makampuni mbalimbali, kwa sababu mbinu za kutangaza bidhaa ndizo huamua ukubalikaji wa bidhaa yenyewe.

Kwa mfano ua la waridi (rose) litabaki kuwa hivyo katika mataifa na tamaduni mbalimbali, lakini rangi za maua hayo zinakuwa na maana tofauti tofauti kutoka utamaduni, taifa moja kwenda jingine. Wajapan wanapendelea maua hayo yenye rangi nyeupe wakati watumiaji kutoka Hong Kong wanapendelea kutumia maua hayo ya rangi nyekundu

Mtu anapotaka kununua gari, rangi inatajwa na wataalamu wa masuala ya biashara kuwa inashika nafasi ya tatu katika orodha ya vigezo vya bei  na ubora . Rangi pia ina umuhimu mkubwa sana katika ujenzi wa nembo ikiwemo logo, ufungaji na uonyeshaji . 

Mtaalamu na mtafiti wa mambo ya masoko, Wagner kupitia taasisi yake ya utafiti wa mahusiano ya rangi na biashara, ijuliakanayo kama Wagner Color Research Institute, alijaribu kuthibitisha dhana yake  maarufu, ‘Colors are associated with certain images’ (rangi inaambatana na taswira fulani). Wagner alitumia kampuni inayoendesha migawaha iitwayo Wienerschnitzel yenye matawi zaidi ya 350 katika nchi ya Marekani. 

Wagner aliishauri kampuni hii kuongeza rangi ya njano kidogo katika rangi zinazopamba majengo ya migahawa yao ili kuwasilisha ujumbe kuwa kampuni hiyo kupitia matawi yake inauza vyakula vya bei rahisi. Baada ya kubadilisha rangi, kampuni hiyo iliripoti ongezeko la mauzo kwa asilimia saba.

Kiujumla rangi zinaambatana na taswira fulani  kila inapoonekana na kufikiriwa katika fikra za mteja. Kwa mfano rangi ya bluu mahali pengi huambatana na maana na taswira ya utajiri, uaminifu na usalama. Ndio maana ukifuatilia kwa umakini utagundua kuwa benki nyingi zinapenda kutumia ama kujumuisha rangi ya bluu katika nembo na machapisho yao. 

Hii inaingiza taswira miongoni mwa wateja wa mabenki hayo kuwa, benki ipo imara (utajiri mkubwa), ina umaninifu, (hivyo akaunti zake haziwezi kufanyiwa hujuma), na usalama, (kimbilio sahihi la kutunzia hazina zake). Wakati rangi ya njano inabeba mwonekano wa kitu cha bei rahisi

Wasimamizi wa masuala ya masoko katika makampuni na biashara wanapaswa kufahamu maana tofauti tofauti zinazoambatana na rangi ambapo maana hizo zitawezesha kugawanya na kupoka fursa mbalimbali za kimasoko kwenye jamii na tamaduni mbalimbali. Muunganiko wa rangi katika kufungasha bidhaa nao una umuhimu mkubwa sana ili kuwateka wateja.

Upo mfano mwingine wa kampuni ya kutengeneza vifaa vya kompyuta ya Apple kupitia bidhaa zake za iMac inafungasha kutumia mwunganiko wa rangi tano ambazo zina maana tofauti tofauti katika mataifa mbalimbali.  Rangi hizo ni kijani, dhahabu, nyeupe, bluu na njano. Bidhaa za iMac zinapoingia Taiwan zinatafsiriwa kuwa ni amani, rafiki (kijani), zisizo na madhara (bluu na nyeupe), endelevu (dhahabu), zinazosisimua, zinazofanya kazi kwa haraka na kwa ufanisi (njano). 

Muunganiko huo wa rangi unapoingia China tafsiri inakuwa ni nyingine kabisa lakini bado tafsiri inaisaidia na kuiwezesha kampuni kuuza bidhaa zake vizuri. Kule china bidhaa za iMac huleta maana ya; amani (kijani), nzuri na zinazoleta urembo (njano) wakati nyeupe huwakilisha vitu vilivyo katika mpangilio na vinavyofafanulika.

Kuna changamoto kubwa inayowakabili wajasiriamali wa Tanzania hasa katika wakati huu ambao tupo katika jumuiya ya Afrika Mashariki. Namna bidhaa zetu zinavyotengenezwa na kufungashwa zinaamua sana jinsi zinavyoweza kushindana katika masoko ya kimataifa. 

Hata wafanyabiashara wadogo wadogo katika maduka na vibanda vyao ni vema sana wakawa na ufahamu wa namna ya kupaka rangi zitakazowavutia wateja na kuongeza uhakika wa kushinda changamoto za kiushindani!



Mwanafunzi Afariki Ndani Ya Chumba Cha Nyumba Ya Kulala Wageni Akitolewa Mimba

 
MWANAFUNZI  wa kidato  cha tatu katika shule ya Sekondari ya Tongoni nje kidogo ya jiji la  Tanga,  (jina tunalihifadhi) amekutwa amekufa ndani ya nyumba ya kulala wageni alikopelekwa kutolewa mimba bila mafanikio.
Kwa mujibu wa habari zilizopatikana na kuthibitishwa na Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Tanga, Constantine Massawe mwanafunzi huyo alikutwa amekufa juzi katika nyumba ya kulala wageni iliyopo barabara ya 21 jijini Tanga.
Mmoja wa wahudumu wa nyumba hiyo ya kulala wageni ambaye aliomba jina lake lihifadhiwe alisema kwamba mwanafunzi huyo aliingia saa 4.00 asubuhi siku ya tukio akiwa ameambatana na kijana mmoja wakakodi chumba.
“Baadaye alikuja mwanaume mmoja wa makamo ambaye alituuliza kama wameingia mwanafunzi huyo na mwenzake, tulipomwonyesha chumba  walichoingia naye akakodi chumba cha jirani ndipo tukaona wote wakijifungia kwenye chumba kimoja,” alisema mhudumu.
Mhudumu huyo alisema baada ya muda wa saa moja, mvulana na mzee huyo wakaaga kwamba wanatoka huku wakisema kwamba msichana amebaki chumbani akiwa amepumzika. Akithibitisha habari hizi, Kamanda Massawe alisema taarifa ya tukio hilo ilitolewa na mhudumu wa nyumba hiyo ya kulala wageni katika Kituo cha Polisi cha Chumbageni Jijini Tanga.
“Tatizo ni kwamba nyumba hii ya wageni wahudumu wake hawakuwapa wageni hao daftari ili waorodheshe majina yao hivyo inakuwa vigumu  kuwafahamu,” alisema Kamanda Massawe na kufafanua kuwa alifariki akitolewa mimba ya mwezi mmoja.
Kamanda Massawe alisema mpaka sasa hakuna mtu aliyekamatwa na kwamba polisi wanaendelea na uchunguzi ili kuwabaini waliohusika na kifo hicho.


Raisa Said, Tanga